MAHAKAMA YAIANDIKIA WIZARA KUREJESHA MALI ZA MELI YA MAGUFULI

Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli.

Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, imeiandikia barua Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi kwa ajili ya kurejesha mali ikiwamo meli ya Tawariq 1 na  zaidi ya Sh. bilioni mbili za tani 296.3 za samaki kwa raia wawili wa China.
Watu hao ni Hsu Tai na Zhao Hanquing walikamatwa wakivua samaki katika Ukanda wa Kiuchumi wa Bahari ya Tanzania bila kibali.

Kwa mujibu wa barua hiyo iliyosainiwa na msajili wa Mahakama hiyo ya Desemba 17, 2014, imeitaka Serikali kurejea ahadi, kupitia hati ya kiapo iliyotolewa na Godfrey Nanyaro, Dk. Charles Nyamlundana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi.

Kwa mujibu wa barua ya msajili huyo, kiapo kinasema endapo washtakiwa hawatakutwa na hatia mahakamani Serikali italipa gharama za samaki waliokutwa nao wa tani 296.3 za Sh. 2,074,249,000 ndani ya siku 30 tangu kuachiwa na mahakama.

Chanzo cha NIPASHE kinaeleza kwamba mbali na barua hiyo, Mahakama Kuu, imeambatanisha nakala ya amri ya kuuza samaki hao uliotolewa Desemba 11, mwaka 2009 na Jaji Radhia Sheikh, hukumu ya kuwaachia huru ya Mahakama ya Rufani na Hati ya Mkurugenzi wa Mashitaka Nchini (DPP) ya kuwafutia mashitaka Agosti 14, mwaka 2014.

Septemba Mosi, mwaka huu, upande wa utetezi uliwasilisha barua ya kudai vielelezo hivyo, mbele ya Msajili wa mahakama hiyo.

Katika barua hiyo utetezi wanaomba kwamba mahakama iwarejeshee vielelezo vilivyotolewa katika Mahakama Kuu katika kesi namba 38 ya mwaka 2009 mbele ya Jaji Radhia Sheikh.

Barua hiyo ilivitaja vielelezo hivyo kuwa ni, meli ya uvuvi Tawariq 1 pamoja na Sh. 2, 074,249,000 za tani 296.3 za samaki walizokutwa nazo raia hao ambavyo vilitolewa Oktoba Mosi, 2009 mbele ya Jaji Sheikh.

Awali, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, iliamuru serikali ya Tanzania kulipa meli ya uvuvi pamoja na samaki waliokamatwa miaka mitano iliyopita vyote vikiwa na thamani ya Dola miliobi 3.2  baada ya kuwaachia washtakiwa wawili raia wa China, waliokuwa wanakabiliwa na kesi hiyo.

Wakili wa utetezi Kapteni Ibrahim Bendera, alisema baada ya mahakama kutoa amri hiyo, meli iliyokamatwa na wateja wake ilikuwa na thamani ya Dola milioni 2.5 na samaki waliokutwa nao washtakiwa hao walikuwa na thamani ya Dola 720,000.

Agosti 22, mwaka huu Hakimu Mkazi Mkuu, Mfawidhi, Isaya Arufani alisoma uamuzi wa kuwaachia huru wachina hao pamoja na mambo mengine mahakama yake iliamuru serikali kulipa mali hizo pamoja na hati zao za kusafiria.

0 comments: