MAITI YASAFIRISHWA JUU YA KERIA INGIA HAPA

Jeneza lenye mwili wa marehemu likiwekwa vizuri kwenye keria ya gari tayari kwa safari.

DUNIANI kuna matukio! Tofauti na utaratibu uliozoeleka, katika hali ya kushangaza, wanandugu wamelazimika kusafirisha maiti juu ya keria ya basi kutoka Arusha hadi Lushoto, Tanga kutokana na ukata.

Tukio hilo lilitokea hivi karibuni ambapo chanzo kilieleza kuwa, wanandugu hao ambao hawakuwa tayari kuanika majina yao, walifikia hatua hiyo ili waweze kuenea kwenye basi moja aina ya Toyota-Coaster kwenda Lushoto, mkoani Tanga.
Waombolezaji wakiupandisha mwili wa marehemu (ndani ya jeneza) juu ya gari.

“Waliona kama wangeweka maiti ndani ya gari, wangelazimika kutoa siti mbili hivyo wasingetosha, baadhi ya ndugu walishauri kwamba mwili wa marehemu uwekwe juu ya keria ili waombolezaji waweze kuenea,” kilisema chanzo.
Chanzo hicho kilizidi kushusha data kuwa, kabla ya wanandugu kukubaliana kusafirisha juu ya keria mwili huo, uliibuka ubishani mkubwa kwani kuna baadhi waliafiki kitendo hicho lakini wengine hawakuafiki.“Kuna ambao walikataa na kusema si jambo la busara kuiweka maiti juu ya keria lakini mwisho wa siku walizidiwa kwa hoja na wale walioshauri iwekwe juu kwani tatizo lilikuwa kwenye fedha za kukodi gari jingine.

“Walishajikusanya kusanya hadi dakika za mwisho, fedha walizopata zilitosha kukodi gari moja hivyo hawakuwa na jinsi japo ambao hawakuafiki, walihofia kuwa huenda wasifike salama huku wengine wakichungulia pembeni kila wakati wakihofu huenda jeneza linaweza kuanguka,” kilisema chanzo hicho.
Hata hivyo pamoja na kutofautiana huko kwa wanandugu, walifanikiwa kusafiri salama hadi Lushoto na kufanikiwa kumpumzisha mpendwa wao.

0 comments: