ZITTO KABWE: KASHFA NNE MBAYA ZAIDI YA ESCROW ZINAKUJA.. JIANDAENI


Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Kabwe Zitto amesema baada ya kukamilisha shughuli ya ufisadi wa Akaunti ya Tegeta Escrow ambayo Sh306 bilioni zilichotwa, kamati yake sasa inaelekeza nguvu katika kashfa nyingine nne.
 
Zitto alisema kamati yake itatumia mwezi huu na Januari kupitia ripoti nne ambazo zina masilahi kwa Taifa, ikiwamo ya utoaji wa vibali vya kuagiza na kuingiza sukari nchini.
 
Alisema ufisadi katika utoaji wa vibali hivyo ni mkubwa kuliko sakata la escrow... “Hili linagusa moja kwa moja maisha ya wananchi, wamiliki wa viwanda na uzalishaji. Tayari tumewaita Bodi ya Sukari tujadiliane kwa kina kuhusu suala hili,” alisema.
 
Mbali na suala la sukari, alizitaja ripoti nyingine kuwa ni ya uchunguzi wa ubinafsishaji wa Benki ya NBC, ripoti maalumu ya Bandari na mikataba ya gesi.
 
“Baada ya kazi ya PAC, tunapumzika, kwani kama unavyojua kazi ilikuwa ngumu, wiki mbili nilikuwa silali. Kwa kuwa tuna ratiba ya wiki mbili. Kwa Desemba na Januari tutaanza kuzifanyia kazi,” alisema Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema).
 
Wiki iliyopita, Bunge lilijadili ripoti ya PAC kuhusu ufisadi katika Akaunti ya Tegeta Escrow na kuhitimishwa kwa kuweka maazimio manane yakiwamo ya kuitaka Serikali iwawajibishe baadhi ya mawaziri na watendaji wengine wakuu huku likitaka pia uchunguzi uendelee kwa wote waliotuhumiwa kupokea fedha hizo kwa njia moja au nyingine.
 
Kauli ya Zitto inakuja wiki moja baada ya wamiliki wa viwanda vya sukari vya Kagera, Mtibwa na Kilombero kutishia kuvifunga kutokana na kuviendesha kwa hasara.
 
Wamiliki hao walisema watafunga viwanda hivyo kutokana na Serikali kushindwa kuzuia uagizwaji wa sukari nchini kinyume cha taratibu.
 
Mkurugenzi wa Viwanda vya Kagera na Mtibwa, Seif Seif alisema uagizaji wa sukari kutoka nje unafanyika kwa ushirikiano wa wafanyabiashara wakubwa na vigogo serikalini kinyume cha makubaliano na hivyo kurudisha nyuma maendeleo ya viwanda.
 
“Tulikubaliana kwamba Serikali iwe inaagiza tani 100,000 kutoka nje lakini sukari inayoingizwa sokoni ni zaidi ya tani hizo. Sukari tunayozalisha katika viwanda vyetu ipo na haina pa kwenda,” alisema Seif na kuongeza:
 
“Leo ukipita katika maduka utakutana na sukari ya kila aina, wafanyabiashara wanaoagiza wanawatumia vigogo serikalini kuingiza sukari wapendavyo, tena bila kulipa kodi,” alisema Seif.
 
Kutokana na hali hiyo, Seif alisema wamelazimika kupunguza wafanyakazi 2,000 na kubakiwa na 5,000 katika Kiwanda cha Kagera, Kilombero imepunguza 3,000 na wamebaki 6,000 huku Mtibwa ikiondoa wafanyakazi 3,000.
 
“Hali ni mbaya, si kama Watanzania wanavyofikiri. Tukifunga kabisa Watanzania wengi watakosa ajira kama ambavyo mnaona wengine wamekosa, hatuwezi kuendelea kufanya biashara ya hasara ambayo Serikali inaihalalisha,” alisema.
 
Mwenyekiti wa Bodi ya Kiwanda cha Sukari Kilombero, Balozi Ami Mpungwe alisema: “Hali ni mbaya, tunaona kuliko kuendelea na hali hii ni bora tusimame kuzalisha sukari.
 

“Serikali kama kweli ina dhamira ya kuvifufua na kuviendeleza viwanda vyetu vya ndani ni lazima kuvilinda na kupiga marufuku uagizwaji holela wa sukari kutoka nje.”

0 comments: